Naibu Spika atoa ya moyoni
Kwa mara ya kwanza Naib Spika wa Bunge la Jamuhuri ya Muungano wa
Tanzania Dk.Tulia Ackson amezungumzia shutuma dhidi yake za kutumiwa na
Ikulu kuongoza Bunge
Kadhalika, Naibu Spika amezungumzia madai kutoka kwa baadhi ya watu kwamba alimshitaki Spika Job Ndugai kwa vigogo wa nchi.
Dk. Tulia amesema kufuatia
matukio yaliyotokea kwenye vikao vya Bunge lililopita ambalo wabunge
kutoka vyama vinavyounda Umoja wa Katiba (Ukawa) walisusa.
Wabunge hao kutoka vyama vya Chadema, CUF na
NCCR-Mageuzi pia waliwasilisha hoja wakitaka kung’olewa kwa Naibu Spika
kwa kumtuhumu anatumiwa na Ikulu kuubana mhimili wa bunge na kuendesha
vikao vyake kwa misingi ya kupendelea wabunge wa Chama cha Mapinduzi
(CCM).
Dk. Tulia alizungumzia pia maoni ya Spika
Ndugai juu ya sakata la mkataba wa Jeshi la Polisi na Kampuni ya
Enterprises (Ltd) juu ya kufunga vifaa vya kuchukua alama za vidole
kwenye vituo 108 nchini.
Katika taarifa hii iliyo kwenye mfumo wa
maswali na majibu, Dk Tulia pia anazungumza kwa undani sakata lake na
wabunge wanaotoka vyama vinavyounda Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa),
waliosusia Bunge la bajeti kwa kutokuwa na imani na kiongozi huyo
ambaye ni mwanasheria aliyebobea.
Swali: Vipi mahusiano yako ya kikazi na Spika,
ni mazuri? Kwanini baadhi ya watu wanasema kuwa wewe unatumiwa na Ikulu
kuendesha Bunge na wakati mwingine huwa unamshitaki Spika kwa Rais?
Jibu: Mahusiano yangu na Spika yako vizuri.
Niseme tu kwamba Rais anateua wabunge 10 na anateua mawaziri na watu
wengine, lakini hana mamlaka ya kuteua Spika na Naibu Spika, kwa hiyo
watu wanasahau wanadhani kwamba unaibu Spika nimepewa sijui, nimeteuliwa
na Rais, hapana, ubunge nimeteuliwa na Rais, unaibu spika
nimechaguliwa na wabunge kama ambavyo angeweza kuchaguliwa yoyote
aliyekuwa anagombea.
Kama nilivyokwambia tulikuwepo wawili
tuliokuwa tunagombea, wote tulikuwa na sifa, lakini ikatokea mimi ndo
niliyeshinda kwa asilimia 71.
Kwa hiyo watu wanadhani hii nafasi nimepewa na Rais, hapana, nimechaguliwa na kura za wabunge kwenye hii nafasi.
Lakini sasa mtu akisema napigiwa simu na Rais,
hivi nchi hii kuna mtu ambaye hataki kupigiwa simu na Rais? Ama hapendi
kupigiwa simu na Rais? Kwa sababu hata kama napigiwa ama sipigiwi, yeye
anayenituhumu ana shida gani nalo hilo?
Ana tatizo gani? Ni sawa tu nikipigiwa na yeye kama mbunge, kwanini anapata tatizo kwamba napigiwa simu?.
Lakini tatizo ninaloliona ni kusema Naibu
Spika, anapiga simu Ikulu kumsemea Spika, mimi namsemea Spika nimekuwa
msemaji wake ama namsemea nini? Unajua kuna watu ni wazuri katika
kuchonganisha watu, yeye kama anajua kwamba Spika huwa anasemewa,
ameongea na Spika ndo akamwambia hivyo? Kwamba Naibu Spika huwa
ananisema?
Kwa hiyo mimi nisingependa kwenda huko kwa
sababu najua watu wengi tu wanatunga maneno, ni sawa na hili ulilosema
kwamba Spika anapata taarifa za kuhusu madawati kwenye mtandao wa wa
kijamii wa Watsapp (Sh. bilioni sita, ambazo Bunge lilipeleka kwa Rais
ili zinunue madawati), nani alienda kumhoji Spika akamwambia kwamba
amepata taarifa kwenye Watsapp? Anajua mimi nilitumwa na nani kwenda
Ikulu?
Hajui lakini anajisema tu, sasa mimi sioni
sababu ya kumtafuta kumjibu kumwambia unajua mimi nilitumwa na Spika
kwenda Ikulu, siwezi kwenda huko kwa sababu naona tu ni mtu anatunga
taarifa kwa sababu anataka kuziamini.
Kwa hiyo habari hizo za ugomvi ni watu
wanatunga kwa sababu wanazojua wenyewe, lakini mimi huko nisingependa
kwenda kwa sababu watu wanatunga mambo mengi, hilo ni mojawapo.
Swali: Ulichukuliaje uamuzi wa wabunge kusema hawana imani na wewe?
Jibu: Katika hali ya kawaida ukiwa kiongozi
lazima ujifunze kuishi na watu wa kila aina, wakiwa pale ndani wakiwa
kundi wakitoka ndo mtu unaona sijui wamefanyaje, lakini mimi ndiye
ninayeshughulika na mambo yao ya kila siku ofisini pale.
Kwa hiyo yale nayowafanyia ofisini hawayakatai, hawasemi barua zao haziwezi kusainiwa na Naibu Spika na ruhusa wanaomba kwa Naibu Spika.
Kwa hiyo yale nayowafanyia ofisini hawayakatai, hawasemi barua zao haziwezi kusainiwa na Naibu Spika na ruhusa wanaomba kwa Naibu Spika.
Kuna vitu wanafanya kwa jumla ni sawa (uamuzi
wa wabunge wote wa Ukawa kutoka nje ya Bunge), ikija masuala yao ya
mbunge mmoja mmoja, maombi sijui anapeleka wapi, hawezi sema maombi
yangu sitaki yasomwe na Naibu Spika.
Lakini kwa sababu kama nilivyosema lile Bunge
ni jumba la siasa, ni jambo jema tu wao kuonyesha msimamo wao lakini
nadhani walichukua hatua nzuri tu kisheria na kikatiba, kwa maana ya
kwamba walichukua hatua ambayo Katiba inatambua na kanuni zinatambua ya
kupeleka hoja kwa Spika ya kutokuwa na imani na Naibu Spika.
Kwa hilo walifanya vyema kwa sababu katiba na
kanuni inatambua kwamba waliokuchagua kuna wakati wakawa wamekuchoka ama
hawakubaliani na namna wewe unavyowaendesha.
Kwa hiyo wewe umechaguliwa kwa kura
watakuondoa walewale waliokuchagua, kwa sababu hiyo siyo jambo ambalo
ningesema linanitisha ama limenitisha kwa wao kupeleka hoja kwa sababu
ni jambo la kawaida katika uongozi.
Unaweza kuwepo pale ama ukaondolewa na wale waliokuchagua.
Unaweza kuwepo pale ama ukaondolewa na wale waliokuchagua.
Lakini kutokutishwa huko kunatokana na
kuelewa kwamba katiba imetaja, kanuni zimetaja, ni jambo linaloweza
kutokea, lakini siwezi kusema kwamba kura zingetosha ama zisingetosha
kwa sababu mimi nina kura moja tu.
Na walionipiogia kura kushika hiyo nafasi ni
haohao wangeweza kuniondoa kwa hiyo siwezi kusema nina uhakika
wasingeweza kuniondoa kwa sababu kura unayo moja, hayo ndio mazingira,
lazima uwe tayari vinginevyo kama hujajiandaa, unaweza pata shinikizo la
damu.
Swali: Ulikuwa unajisikiaje ukiona wabunge wa Ukawa wanavyotoka bungeni?
Jibu: Unajua ukiwa kiongozi lazima uone namna
ambavyo jambo linalotakiwa kwisha lazima liishe, hili bunge halikuwa la
kawaida kwamba unasema hoja hii tuiache tuimalize kesho, hoja ya bajeti
ikiwa mbele hakuna hoja nyingine unaweza kuleta mbele.
Lingekuwa bunge jingine huenda mambo yangekuwa
tofauti, kwa sababu hoja ya serikali lazima iishe, walivyokuwa wanatoka
nilikuwa naona sawa, kwa sababu, sababu zao mimi binafsi sijazisikia
kutoka kwao, ningezisikia kama hivi nimekaa na wewe hapa, ningesema
sababu walizokuwa wanazitoa ni hizi.
Sasa sababu zao nimeziona tu kwenye vyombo vya habari, nisingeweza kuzisemea kwamba wao walikuwa na sababu gani haswa za kutoka.
Lakini katika uendeshaji wa Bunge na haswa
mabunge mengine ya Jumuiya za Madola, kufanya walichofanya kama
wangetoka mara moja ama mara mbili ama kutolewa siyo jambo la ajabu,
wameshatolewa mara nyingi tu huko nyuma, jipya ni hilo la kutoka kila
siku.
Ila sasa ukitoka unaowakilisha wanakosa
mwakilishi, laiti ningejua sababu zinazowatoa ningejua kanuni fulani
inalalamikiwa, ama kanuni fulani wanadhani nimevunja, badala ya kupeleka
hoja kwa kamati wanaibeba wao wenyewe, sasa siwezi kwenda huko kwa
sababu sijui wanacholalamikia.
Swali: Umewahi kuwaita kuzungumza nao?
Jibu: Unawaita kwa suala lipi? Labda hata wao
wangeitwa waulizwe kwanini wanatoka ama waliwahi kuleta malalamiko yao
rasmi, au kunifuata?
Swali: Vipi mahusiano yako na wabunge yako vizuri?
Jibu: Wabunge tena wote, hata hao wa
upinzani, wakiwa kundi ndo wanatatizo kwamba wametoka pamoja, siyo
kwamba mmoja mmoja hamuwasiliani ama hamuongei, hapana.
Swali: Kumekuwa na hoja kwamba umepewa
nyadhifa nyingi kwa kasi, tunajua ulikuwa mhadhiri, ukawa Naibu
Mwanasheria Mkuu wa Serikali, ukachukua fomu kugombea uspika kabla
hujateuliwa kuwa mbunge na ukagombea nafasi ya Naibu Spika ukaipata,
hoja inakuja ni lini ulichukua kadi ya CCM?
Jibu: Hiyo ndo siasa moja kwa moja sasa naweza
kusema, mtu anaweza kuona matatizo ya mtu mwingine, ama wanasema anaona
boriti kwa mwenzie wakati yeye ana kibanzi.
Mimi sioni hizo ni kasi, ni hatua tu, kuwa
Naibu Mwansheria Mkuu ni kuteuliwa na Ras, nilipoteuliwa kuwa wapo
wanaojua na wengine hawakujua, hawakujua kama nafanya kazi ama nalala
nyumbani, magazeti mengine yakawa yanaandika yanashangaa, sijui wao
walitarajia nani ateuliwe.
Nikaja kuchukua fomu ya unaibu spika, wengine
pia wakashangaa, wakaona huyu sijui ana matatizo gani, wakasema anatamaa
na vitu kama hivyo lakini nisingekaa mahali kufikiria watu wanasemaje,
wanafikiri nini? La msingi ni mimi kukaa na kuona nataka nini ndio
nitakachofanya.
Sasa kusema kwamba kasi imewatisha watu na
kusema sema, unajua mle bungeni kuna wabunge wa aina tano, wanaotoka
kwenye majimbo, Baraza la Wawakilishi la Zanzibar, wanawake wanaoletwa
na chama kulingana na kura (viti maalum), Mwanasheria Mkuu na sisi
tulioteuliwa na Rais.
Kwa kundi la wanawake kwa kuwa ni mfumo wa
vyama vingi kila chama kina utaratibu wake, tume (Tume ya Taifa ya
Uchaguzi) wanataka majina, yanapatikana vipi ni kazi ya vyama, vyama
vingine wanafanya kura za maoni, wanaoshinda wanaendelea, hao ni wa
majimbo, wengine wa viti maalumu pia walifanya kampeni na zilizisikika,
vyama vingine vilileta orodha majina ya watu ambao mpaka yanatangazwa na
tume walikuwa na kadi za CCM.
Wao waliwapata wapi? Walichukua fomu saa ngapi
za kujiunga na vyama vyao na kadi za zamani walirudisha lini? Hao ni
wengi sihitaji kuwataja majina ndo maana nasema mtu ana kibanzi anaona
boriti la mwenzake.
Kwa hiyo hoja ya mimi nilipata lini kadi ya
CCM ni suala la chama changu kuliko mtu mwingine yoyote, kama chama
kiliona naweza kugombea uspika wewe kwamba nilipata kadi lini una tatizo
gani nalo?
Kama nilipata asubuhi kadi nikagombea mchana
wewe linakuhusu nini? Kama chama changu kiliona ni sawa wewe una tatizo
gani? Kwa sababu huo ni utaratibu wa chama changu, wewe chako pia kina
utaratibu wake ambao hakuna anayekuuliza kwa hiyo ni mazingira kama
hayo.
Nadhani tutafika mahali tuanze kujadili mambo
ya msingi kuliko ambayo siyo ya msingi, hata hili la mimi nilichukua
kadi lini sioni kama lina msingi.
Swali: Suala la wewe kuwa Naibu Spika ambaye hutokani na wabunge limekuwa likiibua maswali mengi, hali hiyo inatokana na nini?
Jibu: Ni kweli imezoeleka kwamba Naibu Spika
anatokana na wabunge, lakini mambo mengi siku hizi yamebadilika, huko
nyuma pia katiba ilikuwa inataka Spika ni lazima awe mbunge.
Ikaja ikabadilika, kwa hiyo sasa hivi mtu
yoyote anaweza kuwa Spika, kikubwa tu apitie kwenye chama, lakini
anaweza kuwa mtu yoyote, Naibu Spika ndiyo katiba inasema lazima awe
Mbunge.
Kwa hiyo utagundua Naibu Spika anafanya kazi
chini ya Spika, kama Spika anaweza kuwa mtu yoyote na na akaongoza
vikao manake yeye ndo kiongozi wa mhimili.
Sasa kama kiongozi wa mhimili, katiba
inatambua kwamba anaweza kuwa mtu yoyote, ilimradi awe na vigezo vya
kuwa mbunge, mimi sioni kwa nini watu wanapata tabu na hili la Naibu
Spika, kwa hiyo msingi ni huo, mabadiliko huwa yanachukua muda kuyazoea,
mimi naamini tutafika kama jamii kuona zaidi mtu anafanya nini kuliko
kuona mambo mengine kwa sababu yapo mengi ambayo watu wanaangalia
unapokuwa kwenye nafasi.
Mtu ataangalia umri, ataangalia huyu ni
mwanamke au mwanaume, akiwa mwanaume wanaona kwamba ni jambo la kawaida,
akiwa mwanamke tayari mjadala utaanza, mwanamke kufanya kile lakini
hakuna mwanaume atajadiliwa, kwa hiyo mimi naamini baada ya muda haya
yote yatakaa vizuri badala ya kujadili mtu atajadili utendaji ama kazi
anazofanya.
Swali: Kulikuwa na malalamiko kwamba, suala la
Lugumi ulilifunika na likuwa halijaisha, hivi karibuni Spika kasema
litarudi bungeni, maoni yako ni yapi juu ya namna ulivyolimaliza?
Jibu: Spika akishaongea mimi siwezi kufanya
mjadala juu yake kwa sababu yeye ni kiongozi wangu. Kwa hiyo juu ya
ninaonaje, haijalishi tena kwa sababu mkuu wangu keshaongea, kwa sasa
haijalishi mimi naonaje.
Swali: Pia kumekuwa na malamiko kwamba
ulimzunguka Spika ukarudisha fedha za Bunge kwa Rais (Sh bilioni sita)
bila kumshirikisha, ukweli wa hili ukoje?
Jibu: Kwa kawaida kuna bajeti ambayo inatokana
na maombi maalum, inapotokea jambo lililoombewa fedha limeisha, kuna
utaratibu wake.
Kwa kawaida kama jambo limeisha yule
alipelekewa fedha anaweza kumuomba waziri(Waziri wa Fedha) abadilishe
matumizi ama kurudisha kabisa fedha kwamba hili jambo limeisha.
Fedha zile zilipatikana kupitia bajeti
2015/16, mwaka jana kulikuwa na uchaguzi kwa hiyo bunge lilivunjwa
mapema, kwa hiyo wabunge walikuwa hawalipwi mshahara wala posho kwa hiyo
fedha zilitokana na kubana matumizi kwenye maeneo mbalimbali na
nyingine ndo zile.
Ofisa Masuhuri wa bunge ni Katibu wa Bunge,
ndiye anajua fedha zilizoingia, kwa kutojua ndiyo wanadhani kuna chombo
kinatakiwa kushirikishwa kabla ya kutoa fedha.
Mimi hata hizo akaunti za Bunge sizijui na
sijui hata kama zina hela, yawezekana mtu hajui jambo lakini kwa sababu
anajulikana na anajua akisema litaandikwa, basi anasema tu.
source:ipp media
Leave a Comment