Mrema awapa siku 7 polisi wala rushwa
Mwenyekiti wa bodi ya Parole Augustine Mrema amewapa siku saba madera wa pikipiki za kupakia abiria maarufu kama "bodaboda" wa wilaya ya kinondoni kumpelekea majina ya askari wa jeshi la polisi wanao omba rushwa ili ayapeleke kwa Rais Magufuli
Mrema aliyasema hayo jana alipokutana na Chama
cha waendesha bodaboda na bajaji wa wilaya ya Kinondoni ambapo
walimweleza kuwa, moja ya kero inayowakabili ni kuombwa rushwa na
polisi.
Baada ya kuelezwa jambo hilo, Mrema alijibu:
“Si mnawajua polisi wanaowaomba rushwa, sasa nataka muwaandike katika
karatasi majina yao ndani ya siku saba, namba yake hata ikiwekezekana
mpigeni picha, halafu mniletee ofisini kwangu ili nianze nao kazi.”
Kuhusu bodaboda kutoingia mjini, Mrema
alimtaka Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda, kutoa maelezo ya
kutosha kuhusu hali hiyo wakati eneo la Posta kuna kituo cha madereva wa
bodaboda.
“Ndani ya siku saba, nitazifuatilia zile
bodaboda zilizopaki kituo kilichopo karibu na kituo cha mafuta kilicho
karibu na Ofisi za Posta katikati ya Jiji ili nijue ni za nani? Na kwa
nini zinapaki mjini wakati kuna zuio,” alisema Mrema.
Mrema pia aliwataka madereva bodaboda wote
nchini kutokubali kutumiwa na wanasiasa wakati wa maandamano wala wakati
wa uchaguzi, bali wajielekeze katika kufanya kazi za maendeleo.
Alisema uchaguzi mkuu ulishamalizika na
kilichobakia kwa sasa ni kumsaidia Rais Magufuli katika kuleta maendeleo
ya nchi kwa kuwa yeye ndiye Rais na hakuna mtu mwingine.
Mrema alisema ameanza kutatua kero za
waendesha bodaboda kwa sababu amepewa kazi ya kuongea na vijana ili
kuondoa makosa ambayo yatawafanya kupelekwa mahabusu.
Alisema kwa sasa vijana wanakamatwa ovyo na
kupelekwa vituo vya polisi na mwishowe kupelekwa mahakamani na
kuhukumiwa na kwamba hali hiyo inaongeza idadi ya mahabusu.
Akielezea sababu iliyomtoa Chama Cha Mapinduzi
(CCM) na kuhamia NCCR-Mageuzi, Mrema alisema uwapo wa ufisadi ndani ya
chama hicho miaka ya 1990, ndiyo sababu pekee iliyomkimbiza.
“Nilimwambia Lowassa wakati huo kuwa `maji
yameshachemka weka unga tusonge ugali,’ lakini hakunisikia yeye na
mwenzake Sumaye, matokeo yake mwaka 2008, akajiuzulu baadaye nikasikia
amekatwa, leo yupo upinzani na Sumaye, angenisikiliza wakati ule haya
yote yasingemkuta,” alisema Mrema.
Mrema wakati akiwa Waziri wa Mambo ya Ndani ya
Nchi kuanzia mwaka 1990 hadi 1994, alisifika kwa utoaji wa maagizo ya
kutaka mambo kufanyika kwa siku saba.
Leave a Comment