Mbowe, Lissu wahofia ubunge wao
Mwenyekiti wa chama cha demokrasia na maendeleo (CHADEMA)na mwanasheria Freeman Mbowe wa chama hicho Tundu Lissu wamelazimika kujibu barua walio tumiwa na secretariti ya maadili ya utumishi wa umma wakiofia kuvuliwa ubunge wao
Wawili hao wametakiwa kujieleza kwa
sekretarieti hiyo ndani ya siku 21 kuanzia Agosti 4, mwaka huu kuhusu
kile ambacho Lissu alikieleza jana kuwa ni tuhuma za kuhusika kwao
katika kosa la kukiuka masharti ya hati ya ahadi ya uadilifu kwa
viongozi wa umma.
Licha ya kuikosoa barua aliyotumiwa na
sekretarieti hiyo, viongozi hao wa Chadema ambao pia ni wabunge, Mbowe
Jimbo la Hai na Lissu (Singida Mashariki), watalazimika kuijibu kwa kuwa
wamebaini ni huenda kuna njama inayofanywa kuwavua ubunge wao.
Katika mkutano na waandishi wa habari jijini
Dar es Salaam jana, Katibu Mkuu wa Chadema, Dk. Vincent Mashinji,
alisema kuwa katika barua hiyo aliyodai imeandikwa na Kamishna wa
sekretarieti hiyo, Jaji mstaafu Salome Kaganda, inaelezwa kwamba
viongozi hao wamekiuka masharti ya hati ya ahadi ya uadilifu kwa
viongozi wa umma kwa kutoa matamshi yanayochochea wananchi kutotii
sheria.
Alisema sehemu ya barua hiyo ilieleza kuwa
matamshi hayo yanatokana na maazimio yaliyofikiwa na kikundi cha watu
wachache nje ya Bunge, yakipuuza utengamano, utulivu na usalama wa
wananchi wengine kinyume cha dhana ya maslahi mapana ya umma.
Dk. Mashinji alisema walishtuka baada ya
kupokea barua hiyo na hawakuamini kama imendikwa na Jaji kwa kuwa
“haikuwa na maelezo yoyote ya kile kinachodaiwa kosa, haikutaja tarehe
ya kufanyika kwa kosa hilo, muda au mahali kosa lilipotendeka.”
Katibu Mkuu huyo pia alisema haikutaja vifungu
vya sheria yoyote iliyokiukwa au kuonyesha kama sekreterieti ya maadili
ya viongozi wa umma ina mamlaka ya kisheria ya kushughulikia kosa hilo
na kwamba barua hiyo ilionyesha upungufu wa kitaaluma na kiuandishi.
Akizungumzia barua hiyo, Lissu aliyekuwa
amefuatana na Dk. Mashinji, alisema kuwa kwa namna barua hiyo
ilivyoandikwa, imedhihirisha wazi kuwa Jaji Kaganda hana sifa ya
kuendelea na wadhifa wake huo kutokana na upungufu wake.
Alisema barua hiyo iliyoandikwa na Jaji
Kaganda, ina ishara ya kuwapo kwa njama za kuwafungulia mashtaka
viongozi hao wakuu wa Chadema katika Mahakama ya Maadili kwa lengo la
kuwavua ubunge na kwamba njama hiyo wameibaini na wamejipanga kuikabili.
Lissu alisema barua hiyo inaweza kuwa mtego wa
kuwatafutia vigezo vya kikatiba vya kukosa sifa ya kuwa wabunge kwa
sababu wanaweza kuhesabiwa kuwa ni watovu wa nidhamu endapo watashindwa
kutii agizo la Jaji Kaganda la kujibu barua yake.
“Mojawapo ya vigezo vya kikatiba vya mtu
kukosa sifa ya kuwa ubunge ni pamoja na kuhukumiwa na kupewa adhabu ya
kifungo kwa kosa linaloambatana na utovu wa nidhamu au kwa kuvunja
sheria ya maadili ya viongozi wa umma.
Kwa mujibu wa sheria hiyo, Kamishna wa Maadili
ana mamlaka ya kuchunguza tuhuma za ukiukwaji wa maadili ya viongozi wa
umma na kuunda mahakama (tribunal),” alisema Lissu.
“Mahakama hiyo inaweza kusikiliza tuhuma hizo
na kupeleka taarifa ya mashauri hayo kwa kamishna ambaye atapaswa
kuwasilisha nakala za taarifa hiyo kwa Rais na Spika wa Bunge. Kamishna
wa maadili ndiye atakayeitisha mahakama hiyo baada ya mashauriano na
Mwanasheria Mkuu na Jaji Mkuu,” alieleza Lissu.
Alisema kuwa kwa kuzingatia mazingira hayo ya
kisheria na mazingira ya sasa ya kisiasa kwa vyama vya upinzani, barua
hiyo ina lengo la kutengeneza mazingira ya kisheria yatakayosababisha
kuitishwa mahakama hiyo kwa lengo la kuwakandamiza viongozi hao.
Alisema Chadema imebaini njama hizo na
haitakubali kunyamazishwa na kuruhusu ukandamizaji wa viongozi wake kwa
kutumia kivuli cha maadili ya viongozi wa umma na kwamba wako tayari
kupambana na njama hizo.
JAJI KAGANDA
Alivyotafutwa na gazeti hili jana ili kutoa
ufafanuzi wa maelezo ya Lissu, Jaji Kaganda alisema hawezi kuzungumza
lolote kwa kuwa Lissu ndiyo ameamua kusema hayo aliyosema.
“Yeye (Lissu) ndiye amesema na yeye ndiye
msemaji, kwa hiyo, ‘I have nothing to do with Chadema or any political
party (sina cha kufanya juu ya Chadema ama chama chochote cha siasa,”
alisema Kaganda.
Leave a Comment