Wadaiwa mikopo vyuo vikuu, kuzuiwa kukopa, kwenda nje
Bodi ya mikopo ya Wanafunzi wa Elimu ya juu (HESLB),imetoa orodha ya
kwanza ya wadaiwa 1,091 na kuwataka kujisalimisha vinginevyo watawekewa
vikwazo,vikiwamo kutosafiri nje ya nchi na kutokukopeshwa na taasisi
yoyote ya fedha
Kupitia tangazo la bodi hiyo lililochapishwa
kwenye vyombo vya habari jana, wadaiwa hao wanakabiliwa na adhabu hizo
ambazo ziko kwa mujibu wa sheria iliyoanzisha bodi hiyo mwaka 2004.
HESLB ilisema wakopaji ambao hawarejeshi
mikopo, wanakabiliwa na hatari ya kuchukuliwa hatua za kisheria na
kwamba majina yao yatapelekwa katika taasisi ya kuorodhesha wadaiwa sugu
na watakuwa wamejinyima fursa ya kukopeshwa na taasisi zote za kifedha
nchini, zikiwamo benki na vyama vya kuweka na kukopa (Saccos).
Aidha, taarifa ya HESLB ilisema hatua nyingine
ambayo inakusudia kuchukua dhidi ya wadiawa, kwa mujibu wa sheria, ni
kupeleka taarifa zao za kina Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi, Idara ya
Uhamiaji na balozi zote ili wanyimwe ruhusa ya kusafiri nje ya nchi.
Wadaiwa hao pia watanyimwa kupata udhamini wa
serikali au kudahiliwa kwa ajili ya kusomea shahada za uzamili na
uzamivu kwenye chuo chochote ndani na nje ya nchi.
Mbali na vibano hivyo vinne vitakavyoathiri
mipango na mienendo ya kila siku, wadaiwa pia wanakabiliwa na hatari ya
kukamuliwa fedha zaidi ya kiwango cha deni la sasa.
Kwa mujibu wa tangazo hilo, wadaiwa wa HESLB
watakuwa wakilipa riba ya kila mwezi ya asilimia tano ya deni la mkopo
kwa kila mwaka, mbali na riba ya asilimia tano inayotozwa sasa.
Aidha, wadaiwa wa HESLB watabebeshwa gharama
za kuwatafuta baada ya kukamatwa na wakala wa bodi watakaopewa kazi ya
kuwafuatilia.
Kiasi cha deni la mkopo, kwa kila mmoja wa
wadaiwa hao 1,091, kimeelezwa katika tangazo hilo kwenye gazeti la The
Guardian kuwa kinaweza kupatikana katika ofisi za Bodi.
Mkurugenzi Msaidizi wa Habari, Elimu na
Mawasiliano wa HESLB, Cosmas Mwaisobwa, aliliambia gazeti hili kuwa hadi
sasa mikupuo iliyoiva ambayo wanufaika wanatakiwa kulipa ni Sh. bilioni
480.
Alisema kiasi wanachodai HESLB kutoka kwa
wadaiwa hulipwa kwa awamu na si kwa mkupuo na kwamba wanafanya uchambuzi
wa wadaiwa na wanaolipa kila mwezi.
Akiwasilisha bungeni makadirio ya
mapato na matumizi ya wizara yake kwa mwaka wa fedha 2016/17, Waziri wa
Elimu, Sayansi, Teknolojia na Ufundi, Prof. Joyce Ndalichako, alisema
serikali itaifanyia marekebisho Sheria ya Bodi ya Mikopo ya Wanafunzi wa
Elimu ya Juu ili kuongeza kasi ya urejeshwaji wa mikopo.
Prof. Ndalichako alisema watalazimika
kuifanyia marekebisho sheria hiyo kwa kuwa kiwango cha urejeshwaji wa
mikopo bado hakiridhishi.
Alisema hali hiyo inasababishwa na kuwapo kwa
changamoto za kutokuwapo kwa mikakati thabiti ya ufuatiliaji wa
wakopaji, udhaifu katika sheria ya muundo wa bodi hiyo.
Alisema hakuna sheria inayolazimisha marejesho
ya mikopo kutokana na makato ya mishahara na mwitikio mdogo wa
wanufaika kujitokeza kurejesha mikopo yao pamoja na waajiri kutotimiza
majukumu yao.
"Napenda kuchukua nafasi hii kuwakumbusha
wanufaika kufanya marejesho ili Watanzania wengine wenye mahitaji waweze
kunufaika. Pia nawasihi wenye uwezo mdogo walipe kwa mkupuo mmoja ili
kupunguza utegemezi wa Bodi ya Mikopo kwa serikali," alisema.
Aliongeza kuwa wizara yake imeongeza siku 30
katika siku 60 ilizokuwa imewapa wanufaika wa mikopo kujisalimisha
lakini akaonya kinyume cha hapo majina yao yatatangazwa kwenye magazeti
Leave a Comment